Thursday, March 31, 2016

WADAU WANASEMAJE KUHUSU- MRADI WA USHIRIKI WA WANANCHI KATIKA USIMAMIZI WA MALIASILI

Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira (LEAT) inatekeleza mradi miaka minne wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’, kwa ufadhili kutoka kwa watu wa Marekani kupitia Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID-Tanzania). Mradi huu unatekelezwa katika wilaya za Mufindi na Iringa vijijini katika mkoa wa Iringa. Mradi unatekelezwa katika vijiji 32, na inatarajiwa kuwa zaidi ya watu 6500 watafaidika na mradi. Mradi ulianza mwaka 2014 unatarajiwa kukamilika mwaka 2017.
Katika utekelezaji wa mradi huu, LEAT kwa kushirikiana na Mashirika ya kijamii wanawajengea uwezo wananchi kuhusu ‘Usimamizi wa Maliasili pamoja na Ufuatiliaji Uwajibikaji Jamii. Ilkufikia watu wengi katika makundi mbalimbali LEAT inatoa mafunzo kwa Madiwani, kamati za vijiji na wilaya za maliasili na ardhi; pamoja na wananchi kutoka makundi mbalimbali ya jamii.
Yafuatayo ni baaadhi ya maoni ya wananchi waliofikiwa na mradi:
 
 
Yahya Kutika
Yahya Kutika, akiwa katika bustani ya kupandia miti, kijijini Kiwere
 
Mafunzo ya mradi yamefungua fikra zangu. Nimeanza kufikiri tofauti na nilivyokuwa nikifikiri hapo awali, sasa ninafahamu madhara ya matumizi yasiyo endelevu ya maliasili hususan misitu. Kabla ya mradi, sikujali kuhusu usimamizi wa misitu, na nilikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wanakata miti kwaajili ya kuchoma mkaa. Nilidhani kuwa mimi si wa kulaumiwa kwa kuwa ilikuwa ilikuwa haki kufurahia maliasili zilizopo. Licha ya kuwa watu wengi kijijini wanategemea kuni kama nishati, na vijana wengi wanategemea uuzaji mkaa kama chanzo cha mapato, nadhani kuna haja ya kuangalia njia bora za uvunaji ilitupunguze hatari ya kutoweka kwa rasilimali misitu.
 
Abdul Chang’a
Abdul Chang'a mmoja wa wanakikundi cha uhifadhi mazingira cha Kiwere

Mimi na wake zangu wawili ni wanufaika wa mradi, tulihudhuria mafunzo na tumeshiriki katika utekelezaji wa mradi kwa kuelimisha wenzetu umuhimu wa kutunza msitu wetu, na kuhamasisha upandaji miti katika maeneo yaliyo athiriwa kwa ukataji miti. Tumekuwa mstari wa mbele kuunga mkono jitihada hizi ambazo zinalenga kuiepusha nchi yetu na athari zitokanazo na uharibifu wa mazingira. Huwa ninasikia katika redio namna ambavyo uaharibifu wa misitu umeathiri maeneo mengine duniani, nisingependa hali hiyo itupate. Mimi ni miongoni mwa watu 17 tunaounda kikundi cha uhifadhi mazingira cha Kiwere.
 
Bruno Mpagama
Bruno Mpagama akionesha miche ya miti iliyopandwa na kikundi chao cha Kiwere Hifadhi Mazingira
 
Changamoto kubwa katika usimamizi wa maliasili ni kuwa watu wengi wahatambui wajibu wao, pia nadhani kutofahamu dhana nzima ya ushiriki wa wananchi katika usimamizi wa maliasili. Haya yalidhihirika wakati wa mafunzo ya mradi, ambapo wengi wetu tulikiri kutofahamu dhana hiyo. Nimejifunza kuwa kuto fahamu umuhimu wa kutunza rasilimali hizi za thamani, kuna athari kubwa kwa viumbe hai, kizazi cha sasa na kijacho.
Kutofahamu thamani ya maliasili zetu ndiko kumechangia wananchi wengi wanaoishi karibu na maliasili hizo kuendelea kuwa masikini. Rasilimali hizi zikitunzwa na kutumiwa kwa utaratibu unaofaa zitatunufaisha.
Kupitia mafunzo yaliyotolewa na LEAT nimejifunza kuwa mimi ndiye mdauwa kwanza wa usimamizi wa maliasili, lakini pia nimejifunza sheria na kanuni zilizowekwa ili kurahisisha utelekezaji wa wajibu wangu. Zaidi ya hayo nimefahamu haki na wajibu wangu katika kusimamia utendaji wa viongozi wangu kupitia mfumo wa Ufuatiliaji Uwajibikaji Jamii. Mafunzo haya yamenijengea ujasiri wa kuhoji viongozi wangu kuhusu mapato na matumizi ya mapato yatokanayo na maliasili za kijiji. Mfumo wa Ufuatiliaji Uwajibikaji Jamii unakwenda zaidi ya usimamizi wa maliasili, mfumo huu tutautumia katika kufuatilia katika huduma za jamii, ikiwemo elimu, afya, maji na miundombinu.
 
Mashaka Kilanga- Katibu MJUMUKK
Mashaka Kilanga, Katibu wa MJUMIKK shirika la kijamii linaloshughulikia mazingira, ambalo pia ni miongoni mwa mashirika manne ya kijamii yanayotekeleza mradi
 
Nadhani mradi wa ushiriki wa wananchi katika kusimamaia maliasili umefika kwa wakati katika kijiji chetu. Hapa kijijini tuna msitu wenye ukubwa wa hekta 4904 ambapo kati ya hizo takribani hekta 50 za msitu zimeharibiwa kwa ukataji miti ovyo.
Nathubutu kusema kuwa mafunzo ya mradi wa ushiriki wa wananchi katika kusimamia maliasili ni muhimu sana ilikunusuru harati inayoweza kutokea katika mazingira na viumbe hai. Kabla ya kufikiwa na mradi huu vitendo vya uharibifu wa maliasili vili kithiri ikiwa ni pamoja na ukataji miti usio zingatia taratibu za misitu endelevu, ukataji miti kwaajili ya kuandaa mashamba pamoja na uchomaji misitu ili kufukuza wanyama wanao haribu mazao.
Baada ya kupatiwa mafunzo ya mradi wa Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili, wananchi wamefahamu wajibu wao na wameanza kuchuka hatua ya ulinzi shirikishi katika msitu wa kijiji. Pia serikali ya kijiji imesitisha vibali vya uvunaji msituni, pia inahamasisha wananchi kupanda miti katika kaya zao.
Nawashukuru LEAT na shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani kwa kutuletea mradii huu ambao utanusuru hatari iliyoanza kuukumba msitu wetu.
 
 
Hamza Chang’a
 
Hamza Chang'a, Kiongozi wa kikundi cha uhifadhi mazingira cha Kiwere, akiwa katika bustani ya kupandia miche ya miti
 
Baada ya kuhudhuria mafunzo ya mradi na kuhamasika, mimi na wenzangu 16 tuliamua kuunda kikundi cha kuhifadhi mazingira na tumefanikiwa kupanda miti 45,000 ambayo itapandwa katika eneo la hekta 50 lililo haribiwa kwa ukataji miti. Miti mingine tutaigawa kwa makundi mbalimbali, pamoja na kuendelea kuhamasisha watu kuwa walinzi wa msitu wetu na waendelee kupanda miti ilikukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Nakiri kuwa mkoa wa Iringa tumebarikiwa kuwa na rasilimali misitu na wanyamapori, vitu ambavyo maeneo mengine ya nchi yetu havipatikani, hivyo tunawajibu wa kutunza maliasili hizi ili zituinue kiuchumi, tuondokane na umasikini uliokithiri.
Nimefaidika na mafunzo ya mradi, nimefahamu wizara na taasisi zinazo husika katika uhifadhi na usimamizi wa maliasili. Pia nimazifamahu sheri, kanuni na miongozo inayotumika kusimamia rasilimali hizi, bila kusahau wajibu wangu wa kisheria na kikatiba.
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 

No comments:

Post a Comment