Tuesday, March 22, 2016

SIKU YA MAJI DUNIANI

KAULI MBIU: MAJI BORA, AJIRA BORA

Leo ni siku ya maji duniani, kaulimbiu ‘Maji bora, Ajira bora’. Kauli mbiu hii inaelezea umuhimu wa maji kwa maendeleo endelevu. Ni kweli iwapo maji yatapatikana katika jamii yanaweza kuleta ajira zenye heshima na  staha ambazo zitabadilisha uchumi na maisha ya watu. Upatikanaji wa maji safi na salama kwa maeneo ya mijini na vijini bado ni changamoto kubwa. Kwa maeneo ya mijini inachangiwa na kutokuwepo na miundo mbinu ya maji ya kutosha, uharibifu wa miundo mbinu iliyopo, gharama kubwa za kuunganishiwa maji kutoka mamlaka za maji pamoja na gharama kubwa za kuchimba visima binafsi.
Moja ya vyanzo vya maji ambavyo vianapaswa kulindwa na kutunzwa

Mtoto akitoka kutafuta maji kwaajili ya matumizi ya familia.

Kwa maeneo ya vijijini, changamoto ni kubwa kwakuwa maeneo mengi hayajafikiwa na huduma kutoka mamlaka za maji, gharama kubwa za uchimbaji visima na uharibifu wa mazingira hasa katika vyanzo vya maji. Wakazi wengi wa vijijini wanategemea vyanzo asilia vya maji kama mito, maziwa na chemchem. Lakini wananchi hao ndio huharibu vyanzo hivyo na kuongeza tatizo la upatiakanaji wa maji.

LEAT kupitia mradi wetu wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’ unaotekelezwa katika wilaya za Iringa vijijini na Mufindi, tunaendelea kuelimisha jamii, umuhimu wa kutunza misitu na vyanzo vya maji kwa maendeleo endelevu. Vyanzo vingi vya maji vinaanzia misituni, hivyo misitu inapotunzwa hutunza vyanzo vya maji.

Moja ya matunda ya mafunzo yanayotolewa kupitia mradi huu katika utunzaji na usimamizi wa maliasili misitu pamoja na rasilimali zinazopatikana humo ikiwemo rasilimali finyu ya maji, ni kuimarika kwa utekelezaji wa sheria za usimamizi wa maliasili na maji, zinazosimamiwa na serikali za vijiji. Kabla ya mradi wananchi walikiri kulegalega kwa utekelezaji wa sharia hizo na kusababisha uharibifu wa vyanzo vya maji na misitu. Pia, serikali kwa kushirikiana na wananchi wameweka vibao kuonesha vyanzo vya maji ili watu wasilime katika vyanzo vya maji.

Elimu zaidi inahitajika ili wananchi waelewe madhara ya uharibifu wa mazingira hususan vyanzo vya maji, ilikupunguza adha ya ukosefu wa maji katika jamii. Ukosefu wa maji katika jamii hupelekea wanawake na watoto kutembea umbali mrefu kila siku ilikutafuta maji kwa matumizi ya familia zao. Kazi ya kutafuta maji ni ngumu, licha ya umuhimu wake, ni kazi isiyokuwa na ujira wala kuthaminiwa.
Iwapo upatikanaji wa maji utakuwa wa uhakika, wanawake hawa wangeweza kupata muda wa kujifunza ujuzi ambao ungewasaidia kupata kazi bora zaidi. Ili kuunga mkono agenda ya siku ya Maji Duniani ya mwaka 2016 kila mmoja katika nafasi yake ashiriki katika kutoa elimu ya usimamizi na utunzaji wa vyanzo vya rasilimali maji, kuhakikisha kuna uhakika wa upatikanaji wa maji safi na salama, na kusaidia upatikanaji wa ajira kutokana na maji.

Maji ni muhimu katika kukua kwa uchumi, ustawi wa jamii na viumbe hai. Tanzania imebarikiwa kwa vyanzo vya maji ikiwa ni pamoja na mito, maziwa, maeneo oevu na bahari. Kwa miaka ya hivi karibuni Tanzania imeona kupungua kwa maji kwa kiasi kikubwa katika vyanzo hiyo, na baadhi ya vyanzo vimekauka kabisa. Katika kusaidia athari zaidi, kila mtanzania anawajibika kulinda vyanzo vya maji. 

Duniani wadau wa maendeleo wanaupa kipaumbele mpango wa maji safi na salama kwa maendeleo ya uchumi wa kijani. Kauli mbiu ya mwaka huu imealenga kuonesha jinsi maji yanavyoweza kuunda ajira za heshima katika kuchangia uchumi wa kijani na maendeleo endelevu.

Shirika la dunia linaloshughulikia programu za mazingira, limefafanua dhana ya Uchumi wa Kijani kuwa ni uchumi unaolenga matokeo ya kuboresha ustawi wa binadamu, usawa wa kijamii na kupunguza kwa kiasi kikubwa hatari za mazingira na uhaba wa viumbe hai. Uchumi wa kijani umelenga zaidi kwa maitafa yanayoendelea kwakuwa ndio waathirika wakubwa wa matokeo ya uharibifu wa mazingira.
 
Wanawake na watoto wakitoka kutafuta maji

No comments:

Post a Comment