Saturday, June 25, 2016

LEAT IMEANZA MCHAKATO WA KUZIWEZESHA SERIKALI ZA VIJIJI KUANDAA SHERIA NDOGO ZA USIMAMIZI WA MALIASILI NA MAZINGIRA


Katika kufikia malengo ya mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili, unaotekelezwa mkoani Iringa; Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) imeanza mchakato wa kuziwezesha serikali za vijiji kuandaa sheria ndogo zitakazo waongoza katika usimamizi wa maliasili na mazingira.

Sheria hizo zitasaidia kupunguza uharibifu wa rasilimali misitu na wanyamapori ambazo zipo katika hatari ya kutoweka kutokana na uvunaji haramu.
 
Kutoka kushoto ni Mwanasheria wa Wilaya ya Mufindi bwana Simon, Afisa Mazingira wa LEAT, Edina na Mwenyekiti wa kijiji cha Ludilo
 

Kabla ya kuanza utekelezaji wa mradi katika wilaya za Iringa na Mufindi, mkoani Iringa; LEAT ilifanya utafiti juu ya kiwango cha ushiriki wa wananchi katika usimamizi wa maliasili, pamoja na mambo mengine katika utafiti huo LEAT ilibaini kuwa baadhi ya vijiji havikuwa na sheria ndogo ambazo zingetumika kusimamia maliasili na mazingira. Kutokana na hali hiyo LEAT imeanza mchakato wa kuziwezesha serikali za vijiji kuandaa sheria hizo.

Vijiji vitakavyo wezeshwa katika awamu ya kwanza ni vijiji vya Mbweleli, Kinyika na Kinyali kwa wilaya ya Iringa. Vijiji hivi hakiwahi kuwa na sheria ndogo zinazotumika kusimamia maliasili licha ya kuwa na misitu ya asili ya vijiji. LEAT iliziongoza serikali za vijiji na wananchi katika kuunda sheria ndogo za usimamizi wa maliasili.

Wananchi na viongozi wa serikali za vijiji walitoa mapendekezo ya muundo wa sheria hizo, na wote kwa pamoja walikubaliana kuwa LEAT ichapishe sheria hizo na zimepangwa kuwasilishwa kuanzia mwezi Julai, 2016 kwenye mikutano mikuu ya vijiji, ili wananchi wengi wapate fursa ya kuzijadili na kuzipitisha.

Kwa wilaya ya Mufindi, vijiji vitakavyo fikiwa katika awamu ya kwanza ni Kibada, Ludilo na Ikangamwani. Vijiji hivi vina na sheria ndogo zinazo waongoza katika usimamizi wa maliasili, lakini sheria hizo zilikuwa na mapungufu.

LEAT, serikali za vijiji pamoja na wananchi walipitia sheria hizo na waligundua mapungufu. Wananchi na viongozi wa serikali walioshiriki katika mchakato huo walitoa mapendekezo ya maboresho ya sheria.

Sheria hizo zitawasilishwa katika mikutano mikuu ya vijiji kuanzia mwezi Julai, 2016 ili wananchi wengi wapate fursa ya kuzijadili, kuzifahamu na kuzipitisha.

Malengo ya mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili, ni kujenga utamaduni wa wananchi kushiriki katika usimamizi wa maliasili, kuzijengea uwezo jamii za wenyeji katika kuziwajibisha na kuzisimamia taasisi za serikali zenye majukumu ya kuhifadhi na kusimamia maliasili. Mradi pia umelenga kukuza ufanisi katika utekelezaji na usimamizi wa sera na sheria muhimu zinazo husika katika usimamizi wa maliasili, mabadiliko ya hali ya hewa na tabia nchi.

Kwa kuwa rasilimali zilizolengwa zinapatikana vijijini, LEAT iliona vyema kuwa lazima vijiji hivyo viwe na sheria ndogo zitakazo waongoza katika kusimamia kikamilifu maliasili zilizopo katika maeneo yao.

LEAT imekwisha toa mafunzo ya usimamizi wa maliasili kwa wananchi, kamati za maliasili, mazingira, ardhi, maendeleo ya jamii na fedha. Viongozi wa serikali za vijiji, Madiwani na Maafisa maliasili na ardhi, nao wamepatiwa mafunzo hayo. Makundi hayo yote yamejifunza sera na sheria zinazotumika katika usimamizi wa maliasili. Pia wamejifunza majukumu ya taasisi na idara za serikali zinazohusika katika usimamizi wa maliasili.

Mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’ unatekelezwa na LEAT katika vijiji 32 vya wilaya za Iringa na Mufindi, mkoani Iringa. Mradi umefadhiliwa na Watu wa Marekani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).

 

 

Mwanasheria wa LEAT, Hadija Mrisho akiongea na wananchi wakati wa kujadili muundo wa sharia za usimamizi wa maliasili


Afisa Mazingira wa LEAT, Edina Tibaijuka (anaye watazama wananchi) akifafanua jambo wakati wa mapitio ya sheriandogo za vijiji zinazosimamia maliasili

 
 

Wednesday, June 8, 2016

LEAT YASHIRIKI USAFI WA MAZINGIRA


Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) imeshiriki shuguli za usafi pamoja na wananchi katika kijiji cha Mfyome, wilayani Iringa, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya mazingira duniani.

Timu hiyo pamoja na wananchi walifanya usafi katika Zahanati ya Mfyome na baadaye katika mitaa ya kijiji hicho.

Akiongea wakati wa maadhimisho hayo, Nesi wa zahanati ya Mfyome, bi. Veronica Komba aliishukuru LEAT kwa kushiriki katika maadhimisho hayo ikiwa ni pamoja na kuhamasisha jamii kujenga utamaduni wa kusafisha makazi na mazingira yao.

Bi. Komba alisema kuwa jamii haina budi kujenga tabia ya usafi katika makazi yao ikiwa ni pamoja na kuzingatia kanuni za afya kwa kunawa mikono katika maji churuzi, baada ya kutoka maliwatoni, kuchemsha maji ya kunywa, kuchimba mashimo ya kuhifadhi taka ilikujiepusha na magonjwa ya kuhara na kipindupindu.

“Mtu ni afya, na afya bora inapatikana kwa kuzingatia kanuni bora za afya, kila mmoja asisitize usafi katika kaya yake, ilikuepukana na hatari ya kupata maradhi, kama ilivyotokea ugonjwa wa kipindupindu katika kata ya Pawaga na kugharimu maisha ya watu”, alisisitiza Veronica.

Kwa upande wake Afisa Mawasiliano wa LEAT, Miriam Mshana aliwapongeza wananchi kwa kushiriki katika maadhimisho ya siku ya mazingira, na kutoa wito wa kujenga utamaduni wa kuishi katika mazingira safi.

Kutokana na kaulimbiu ya mwaka 2016 ya siku ya mazingira duniani ‘Shiriki kufanya dunia mahali bora’, Miriam alisisitiza wananchi kutunza mazingira na maliasili, kwa kufanya hivyo tutakuwa tumefanya dunia kuwa mahali bora kwa binadamu, wanyama, mimea na viumbe hai wengine.

Alisema takwimu mbalimbali zinazotolewa na wadau wa mazingira zinaashiria kuwa dunia imechafuliwa na kuharibiwa kwa kiasi kikubwa; hivyo jitihada za dhati zinahitajika ilikudhibiti hali hiyo.

Vyanzo vya maji vimechafuliwa kwa kilimo, taka na kemikali zitokazo viwandani na migodini, shughuli hizo zimepelekea maji hayo kuto kuwa safi na salama kwa matumizi ya binadamu. Ukataji miti na uchomaji misitu umekithiri na kuchangia katika ongezeko la hewa ukaa na joto nchini.

Miriam pia aligusia suala la ujangili wa wanyamapori, na kusema kuwa ujangili umetishia kutoweka kwa baadhi ya wanyamapori hasa tembo. Alisema uvunaji wa kasi wa tembo unaathari kubwa kwa biashara ya utalii ambao una mchango mkubwa katika pato la taifa.

“Ombi langu kwa wananchi na viongozi wa vijiji mliopata mafunzo ya mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’, kuwa muendelee kuwa mabalozi kwa kuhamasisha usimamizi na uhifadhi wa maliasili zetu, na kutoa taarifa za uharibifu wa maliasili katika serikali ya kijiji”, alitoa wito.

Kijiji cha Mfyome ni moja kati ya vijiji 32 vya wilaya za Mufindi na Iringa, vilivyofikiwa na LEAT kupitia mradi wa “Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’, unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).

 
 
Afisa Mawasiliano wa wa LEAT Miriam Mshana (wapili kutoka kushoto) na Nesi Veronica Komba (wapili kutoka kulia) pamoja na wananchi wakifanya usafi katika Zahanati ya kijiji cha Mfyome
 
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Mfyome wakifanya usafi katika Zahanati ya kijiji cha Mfyome 
Picha baada ya usafi
Baada ya usafi

Mwenyekiti wa kijiji cha Mfyome, Thadei Dunda ( wapili kutoka kulia) akishiriki katika usafi wa mazingira siku ya mazingira duniani.
Wananchi wakisikiliza ujumbe wa utunzaji mazingira uliotolewa na kikundi cha sanaa Mashujaa cha kijiji cha Mfyome
Baadhi ya wanakikundi cha sanaa Mshujaa wakiimba shairi
 
 

Tuesday, June 7, 2016

SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI



LEAT YAWAASA WANANCHI KUSHIRIKI KIKAMILIFU KATIKA UHIFADHI WA MAZINGIRA NA MALIASILI
Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) imewaasa wananchi kushiriki kikamilifu katika usimamizi wa mazingira na maliasili kwa ustawi wa taifa. Nasihi hizo ilitolewa na Afisa Mawasiliano wa LEAT, Miriam Mshana wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani yaliyofanyika kijijini Lugoda Lutali katika ngazi ya wilaya ya Mufindi, mkoani Iringa.
Katika utunzaji wa mazingira, Miriam alisema kuwa uharibifu wa mazingira umechangiwa kwa sehemu kubwa na shughuli za binadamu ikiwa ni pamoja na ukataji miti ovyo, utupaji taka ngumu na zenye sumu ambao umeathiri mandhari ya miji yetu na kuchangia ongezeko la magonjwa ya njia ya hewa, kuhara na kipindupindu.
Miriam alisema, utupaji taka ngumu na zenye sumu karibu na makazi ya watu na vyanzo vya maji, umeleta athari kubwa kiafya kwakuwa kemikali hizo hupenya ardhini na kudhuru ardhi na vyanzo vya maji, hasa kwa wananchi wanoishi karibu na viwanda na sehemu za uchimbaji madini.
 “Inasikitisha kuwa wamiliki wa viwanda vingi na machimbo ya madini wanakiuka sheria ya mazingira lakini pia wameshindwa kuwajibika kwa jamii zinazo wazunguka ambazo ndio wadau wakubwa wa biashara zao, kwa kaidi kuchukua hatua za kuzuia uharibifu wa mazingira hata baada ya athari kutokea”, alisema Miriam. Aliongeza kuwa shirika la LEAT limekuwa mstari wa mbele kwa zaidi ya miaka 20, katika kusimamia mazingira nchini katika sekta ya madini, viwanda, na mazingira kwa ujumla.
Aliongeza kuwa mamlaka zilizopewa jukumu la kusimamia mazingira zimekuwa na uzito katika utekelezaji wa majukumu yake hali hiyo inatoa mwanya kwa watu kukiuka sharia za uhifadhi wa mazingira.
Kumekuwa na malalamiko mengi na hata madhara yaliyowapata wananchi yanayotokana na uzembe makusudi wa utiririshaji wa maji yenye sumu katika makazi ya watu, lakini matukio mengi yanafumbiwa macho.
Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Afya Duniani (WHO) iliyotolewa mwezi Aprili, 2016 inaonesha takribani watu milioni 2 hufa kila mwaka duniani na zaidi ya watu bilioni moja hupatwa na magonjwa yanayo sababishwa na uchafuzi wa mazingira, alisema Miriam.
Iwapo serikali, wananchi na wamiliki wa viwanda na machimbo ya madini, kila mmoja akitimiza wajibu wa kutunza mazingira tutakuwa natekeleza haki ya kuishi, haki ya afya bora na ustawi, kama ambavyo serikali ilivyo ridhia katika mikataba mbalimbali ya kimataifa ikiwemo mkataba wa Stockholm nchini Sweden  na Rio De janeiro nchini Brazil.
LEAT kama taasisi kubwa ya Wanansheria Watetezi wa Mazingira nchini inatoa wito kwa mamlaka za usimamizi wa mazingira na maliasili kutimiza wajibu wao kwakuwa serikali imewaamini na kuwapa jukumu hilo. Kwakufanya hivyo tutakuwa tunaitikia wito wa kaulimbiu ya mwaka 2016 ya siku ya mazingira duniani-‘Shiriki kufanya dunia mahali pazuri’.
Kuhusu usimamizi wa maliasili, Miriam alisema Alisema, uvunaji wa kasi hasa wa misitu umeathiri na kuchangia mabadiliko ya tabia nchi, kuiweka nchi katika hatari ya kuwa jangwa. Uvunaji haramu wa wanyamapori hususan tembo umeipa hasara taifa.
 Aliongeza kuwa kwa mujibu wa ripoti ya Mtaalam Mashuhuri wa tafiti za tembo duniani, Ian Douglas Hamilton, kwa mara ya kwanza mwaka 1976 alifanya utafiti wa angani, Tanzania kwa ujumla ilikuwa na tembo 316,000, ambayo ilikuwa idadi kubwa sana ikilinganishwa na maeneo mengine duniani.
Mwaka 1976, mbuga ya Selou pamoja na maeneo jirani ilikuwa na idadi ya tembo109,000. Utafiti uliofanywa mwaka 2013, ulibaini kuwa mbuga ya Selou ilikuwa  na tembo 13,084 pekee.
 
Takwimu hizo zinaashiria hatari ya kutoweka kabisa kwa tembo katika nchi yetu na itaathiri biashara ya utalii ambayo ilikuwa ikitoa mchango mkubwa katika pato la taifa.
Sherehe za siku ya mazingira duniani zilizofanyika wilayani Mufindi tarehe 3 Juni 2016 na kuhudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Jowika Kasugo, Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe, Asumpta Mshama, Mkuu wa Wilaya ya Mbarali, ; pamoja na mashirika ya TANAPA, WCS, WWF, SPANEST, LEAT na wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Wanging'ombe, Mh. Asumpta Mshama akiongea na wananchi wakati wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani.
 
Kikundi cha sanaa Mapogoro wakihamasisha utunzaji wa mazingira na uhifadhi wa maliasili
LEAT pia iligawa vitabu na vipeperushi kwaajili ya kutoa elimu ya utunzaji wa mazingira na uhifadhi wa maliasili
 
 

Mwananchi akitia saini baada ya kupokea kitabu cha utunzaji wa misitu, kilicho tolewa na LEAT
 
 
 
 
 
 

Saturday, June 4, 2016

VIKUNDI 32 VYA UFUGAJI NYUKI KATIKA WILAYA ZA IRINGA NA MUFINDI VYA PATIWA ELIMU YA UJASIRIAMALI


Vikundi 32 vya ufugaji nyuki vya wilaya za Iringa na Mufindi vyapatiwa elimu ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki ili kuwawezesha kufanya ujasiriamali bora na kuleta tija katika soko shindani la bidhaa za nyuki (asali na nta).

Vikundi hivyo vilipatiwa mafunzo ya siku tatu na Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) kwa kushirikiana na Mtaalamu wa kujitegemea wa Ujasiriamali, Rogasian Mtana. Wanavikundi hao walipatiwa mafunzo kwa nyakati tofauti ambapo walijengewa uwezo wa kutambua asali iliyoiva, urinaji bora (uvunaji wa asali) unaofuata njia za kitaalam na rafiki kwa mazingira pamoja na njia bora za uchakataji asali ilikukidhi viwango bora vya asali na nta.

Katika kuhakikisha kuwa vikundi hivyo vinapata masoko ya asali na nta, ndani na nje ya Tanzania, vikundi vilielekezwa njia sahihi za kufuata ilikupata vibali vya usindikaji ikiwa ni pamoja na kupata kibali kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Chakula na Dawa (TFDA).
Pia walifundishwa namna bora ya uhifadhi, usindikaji na ubinifu wa lebo na alama ambazo hutoa taarifa juu ya viambato, viwango vya ubora, uzito wa asali, tarehe ya uchakataji na ufungashaji na mahali ilipotoka.
Katika kuhakikisha kuwa asali na nta zinaendelea kuwa katika viwango vya juu vya ubora, vikundi vilifundisha njia sahihi za usafirishaji wa bidhaa zao. Pia walijifunza namna ya kutafuta masoko ikiwa ni pamoja na utoaji huduma bora kwa mteja, pia walipewa orodha ya makampuni yanayofanya biashara ya asali na nta.
Ilikuwasaidia wanavikundi kuwa na biashara endelevu na zenye tija, wawezeshaji wa mafunzo walitoa mafunzo ya utunzaji wa fedha na kumbukumbu. Wanavikundi pia walielekezwa namna ya kuandika katiba za vikundi vyao iliwaweze kuvisajili kisheria na kufungua akaunti za benki kwaajili ya kutunza fedha zao.
Mafunzo hayo ya ujasiriamali katika mazao ya nyuki ndio yamekamilisha programu ya mafunzo ya ufugaji nyuki. Awali vikundi hivyo vilipatiwa mafunzo ya ufugaji nyuki pamoja na kupewa mizinga ya kufugia nyuki na vifaa vya kujikinga na nyuki. Kila wilaya ina vikundi 16 ambapo kila kikundi kina watu 22.
Kukamilika kwa mafunzo ya ufugaji nyuki kutasaidia kufika malengo ya mradi ya kupunguza utegemezi wa rasilimali misitu na wanyamapori kwa jamii zinazoishi karibu na rasilimali hizo; kwa kuwapatia vyanzo mbadala vya mapato.
LEAT inatekeleza mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’, kwa kushirikiana na Asasi za kiraia za MUVIMA na ASH-TECH kwa wilaya ya Mufindi; na Asasi za MJUMIKK na MBOMIPA kwa wilaya ya Iringa. Mradi unatekelezwa katika vijiji 32 kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).


Wanawake walioamua kufanya ujasiriamali wa mazao ya nyuki -wakiwa katika kazi za kikundi wakati wa mafunzo
 
 
Wanakikundi wakijadili jinsi ya kutafuta masoko na mbinu bora za utoaji huduma kwa mteja
 
Tutatoka tu: Wanakikundi wakijadili usanifu wa lebo nzuri kwaajili ya asali
 

Mwanakikundi akiangalia chujio ya asali wakati wa mafunzo
 
 
 
 
 Ubunifu: Mmoja wa wanakikundi akisaniu lebo ya asali wakati wa kazi za kikundi za majaribio
Mwanakikundi akichora lebo kwaajili ya vifungashio vya asali
 
 
Washiriki wa mafunzo ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki wilayani Mufindi
 Mshiriki wa mafunzo akiangalia chujio ya asali
Katika picha ya pamoja ni Wanavikundi vya ufugaji nyuki walio hudhuria mafunzo ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki wilayani Iringa