Tuesday, March 8, 2016

SIKU YA WANAWAKE DUNIANI-MACHI 8, 2016


KAULI MBIU- ‘AHADI KWA USAWA’

Leo tarehe 8 Machi 2016, wanawake duniani wanasherekea siku ya yao (Siku ya Wanawake Duniani), kwa kauli mbiu ya ‘Ahadi Ya Usawa’. Kauli mbiu hii inahamasisha watu wote wake kwa waume kuahidi kuwa watachangia kufikia mafanikio ya usawa wa jinsia katika jamii. Kauli mbiu hii inasisistiza watu wote kuchukua hatua mathubuti ilikusaidia kufikia usawa wa jinsia haraka zaidi; kwa kuwasaidia wanawake na wasichana kufikia matarajia yao katika elimu, uchumi, uongozi wa siasa, huduma za jamii pamoja na kuwaheshimu na kutambua tofauti ya kijinsia.

Mwaka 2014, Jukwaa la Uchumi Duniani lilikadiria kuwa itachukua muda mrefu mpaka mwaka 2095 kufikia usawa wa jinsia duniani. Mwaka mmoja baadaye, mwaka 2015 walikisia kuwa kutokana na kasi ndogo ya maendeleo katika kupunguza pengo la usawa wa jinsia litapungua ifikapo mwaka 2133.


Wanawake wa Afrika

Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili katika
kusaidia kufikia Usawa wa Jinsia ifikapo mwaka 2030

Kaulimbiu ya mwaka 2016 inatoa wito kwa watu wote kusaidia kufikia usawa wa jinsia duniani, Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT), wanahamasisha usawa huo kwa kuhakikisha kuwa wanawake wanashiriki kikamilifu katika Usimamizi wa Mali Asili kupitia mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Kusimamia Maliasili’ unaotekelezwa katika wilaya za Iringa Vijijini na Mufindi mkoani Iringa, kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).

LEAT inatambua na kupongeza jitihada kubwa zinazofanywa na wanawake wa Tanzania katika kuchangia maendeleo ya taifa hili. LEAT inatambua kuwa ushiriki wa wanawake katika usimamizi wa maliasili sio tu kuwa ni suala la usawa wa jinsia lakini pia kutoshiriki kikamilifu kwa wanawake kunaathiri ufanisi wa usimamizi wa maliasili.

Kauli mbiu ya mwaka 2016 inatoa wito kwa watu wote kuahidi kuwa watawawezesha wanawake na wasichana kufikia matarajiao yao, imedhihirika kuwa upatikanaji wa vitu muhimu kwa maisha ya wananchi wa vijijini kama vile maji, chakula, nishati-kuni pamoja na dawa, kutawawezesha wasichana kupata muda sawa na wavulana wa kijisomea wakiwa nyumbani, kwa kuwa wasichana watatumia muda mfupi kusaidia mama zao kutafuta kuni, maji, dawa na chakula kwaajili ya matumizi ya familia.

Katika utekelezaji wa mradi wa Ushiriki wa Wananchi katika Usimamazi wa Maliasili, LEAT inatoa mafunzo ya sheria zinazohusika katika usimamizi wa maliasili, pamoja na mafunzo ya Uwajibikaji Jamii (Social Accountability Monitoring) kwa wadau mbalimbali wakiwemo, Madiwani, Kamati za vijiji na wilaya za Maliasili, Ardhi na Mazingira; Mashirika ya kijamii pamoja na wawakilishi wa makundi mbalimbali ya kijamii.

Ilikuhakikisha kuwa wanawake wanashiriki katika kupanga, kuamua na kusimamia maliasili, LEAT inasisitiza kuwepo kwa idadi kubwa ya wanawake wanakaoshiriki katika mafunzo ya mradi, ilikuleta matokeo chanya kwakuwa, iwapo maliasili zitatunzwa, zitasimaiwa na kutumika vizuri mwanamke ndiye mnufaika mkubwa kwa kuwa yeye ndiye mwenyejukumu la kuhakikisha kuwa maliasili hizo (maji, nishati-kuni) na chakula vinapatikana kwa matumizi ya familia na jamii.

Pia endapo maliasili hizo hazikutunzwa, kusimamiwa na kutumiwa vizuri na hatimaye kupungua au kutoweka; mwanamke ndiye anayepata athari zaidi kwa kuwa atalazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji, kuni na chakula kwaajili ya familia.

Elimu zaidi ya usawa wa jinsia inahitajika kutolewa kwa jamii ili kuongeza kasi ya kufikia usawa wa jinsia ifikapo mwaka 2030. Hii imedhihirika katika mafunzo ya mradi unaotekelezwa na LEAT mkoani Iringa. Ushiriki wa wanawake katika baadhi ya vijiji unatia moyo lakini bado kuna changamoto kubwa, elimu inapaswa kuendelea kutolewa ili wanawake wenyewe watambue wajibu na umuhimu wao katika kufikia usawa wa jinsia.

Licha ya kuwa na idadi ndogo ya wanawake wa vijijini katika kushiriki ama kushika nyadhifa mbali mbali za uongozi, wanawake ambao wamepata nafasi katika kamati mbali mbali za maendeleo za vijiji wamekuwa Mabalozi wazuri wanao toa elimu kwa wanawake wenzao pamoja na jamii kwa ujumla.

Mafunzo ya Uwajibikaji Jamii yamewawezesha wanawake kutambua wajibu wao, kuwa na ujasiri wa kuwahoji watendaji wa serikali kuanzia ngazi ya kijiji, kuhusu mapato na matumizi ya fedha za kijiji, pamoja na ubora wa upatikanaji wa huduma za jamii. Wanawake pia wamekiri kuwa mafunzo haya yamewaongezea weledi wa kusimamia ustawi wa familia na jamii zao.

Wanawake na Chanzo Mbadala cha Mapato

LEAT pia imetoa mafunzo ya ufugaji nyuki pamoja na kugawa mizinga ya nyuki bure kwa wote waliopatiwa mafunzo. Ilisisitiza kuwepo kwa uwiano mzuri kati ya wanawake na wanaume wanaoshiriki mafunzo, ili kuondoa dhana ya kuwa ‘ufugaji nyuki ni mradi ya wanaume tu’, pia ni kutoa fursa ya wananchi wanaoishi katika maeneo yenye maliasili kuwa na chanzo mbadala cha mapato, kuliko kutegemea mazao ya maliasili kujipatia kipato.
Wanawake wengi wanatarajia kunufaika na mradi wa ufugaji nyuki na kuboresha maisha ya familia zao, kwani kuna baadhi ya wanawake ndio walezi pekee wa familia, hii ni kutokana na kufiwa na waume zao, kuachika ama kutelekezwa. Mwanamke anapokuwa na vyanzo vya mapato vya uhakika, anakuwa na amani, ujasiri na ari ya kusimamia maliasili za kijiji. Pia mwanamke anapokuwa na uchumi mzuri, kuna uwezekano mkubwa wa familia na jamii yake kufaidika moja kwa moja na uchumi huo.

 Changamoto zinazo kwamisha Usawa wa Jinsia katika Usiamamizi wa Maliasili

Kuna changamoto mbalimbali ambazo zina kwamisha ama kuchelewesha kufikia kwa usawa wa jinsia ikiwa ni pamoja na uelewa mdogo wa dhana ya usawa wa jinsia, jamii kutotambua majukumu ya wanawake na wanaume, mila na desturi kandamizi pamoja na kulega lega katika utekelezaji wa sera na sheria.

Uelewa mdogo wa dhana ya usawa wa jinsia katika kuleta maendeleo imekuwa ni kikwazo kikubwa katika kufikia adhma hiyo. Watu wengi wanadhani kuwa usawa wa jinsia ni wanawake kuacha kuheshimu wanaume pamoja na kuacha mila na desturi zinzazo wataka wanawake kuwa wanyenyekevu mbeley ya wanaume. Ukweli ni kwamba usawa wa jinsia ni kutoa fursa sawa kwa wanawake na wanaume katika kumiliki uchumi, kupata elimu, nafasi sawa katika uongozi na maamuzi pamoja na fursa sawa katika upatikanaji wa haki, huduma za jamii, kuheshimiwa na kuthaminiwa, kwa kuzingatia kuwa binadamu wote ni sawa, haya yanatekelezwa bila kuathiri mila na desturi za jamii husika kwa kuzingatia haki za binadamu.

Kikwazo kingine ni jamii kuto tambua majukumu ya wanawake na wanaume, kutokana na ukweli kuwa mwanamke ndiye mlezi mkuu wa familia, mara nyingi inatokea baba anatelekeza famila na kumuachia mama mzigo wa kulea familia. Mama anapokuwa mlezi pekee wa familia anakuwa na majukumu mawili, kutafuta kipato na kutafuta mahitaji muhimu ya familia, kwa wanawake wa vijijini ni changamoto zaidi kwa kuwa wanawake hupoteza mida mwing kutafuta maji na kuni kwa matumizi ya familia.
Mila na desturi kandamizi ni pale ambapo wanaume wanapoona kuwa mwanamke ni mtu dhaifu asiye stahili kupewa madaraka makubwa, na kuwa ni mtu anayepaswa kuongozwa tu. Licha ya kuwa kumekuwa na mwamko kwa wanawake waishio mijini, changamoto bado ipo kwa wanawake waishio vijijini ambao inadaiwa kuwa ni wengi kuliko waishio mijini.
Pia wanawake wenyewe kutojiamini kuwa wanaweza kutenda mambo makubwa katika jamii, hii inatokana na mila na desturi kandamizi, kuwa mtoto wa kike tangu akiwa mdogo anafundishwa kuwa yeye ni mlezi wa familia lakini si mzalishaji mali.

Kulega lega kwa utekelezaji wa sera na sheria kumechangia kupunguza kasi ya kufikia usawa wa jinsia. Sera na sheria zinaeleza vizuri mipango ya serikali kufikia usawa wa jinsia lakini utekelezaji wake ni hafifu. Kwamfano, sera na sheria ya ardhi inaeleza wazi kuwa kila mtu anahaki ya kumiliki ardhi, lakini cha kushangaza serikali haijafanya jitihada za kutosha kuhakikisha kuwa wanawake wanapewa kipaumbele kwa kuwezeshwa kumiliki ardhi kwa kuwa umiliki wa ardhi unahitaji pesa nyingi, na wanawake wengi ni masikini. Serikali ilipaswa iwawezeshe wanawake hawa kumiliki ardhi kwa kuitoa kwa mikopo nafuu. Ilikufikia usawa wa 50/50 katika ngazi za maamuzi tunapaswa ku hakikisha kuwa kuna usawa katika kumiliki uchumi.

Matumaini ya Kufikia Usawa wa Jinsia

Baada ya mkutano wa Wanawake uliofanyika Jijini Beijing, nchini China mwaka 1995, Tanzania imesaini mikataba mbali mbali ya kimataifa ya kuzuia ukatili wa kijinsia na kukubali kusaidia wanawake kupata fursa sawa na wanaume ilikuharakisha maendeleo.  

Serikali pia imetoa fursa mbalimbali ilikusaidia wanawake kushiriki katika ngazi mbali mbali za uongozi na siasa, kwamfano Tanzania kwa mara ya kwanza ina Makamu wa Rais mwanamke, Mh. Samia Suluhu, pia ilikuwa na mwanamke Spika wa Bunge, Anna Makinda, Mama Asha Rose Migiro alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa kwanza mwanamke; na alishika wadhifa wa juu kimataifa alipokuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Wapo wanawake wengi katika nchi hii waliopata nafasi za juu za uongozi katika siasa kwa upande wa vijijini kuna wanawake wamepata Udiwani na Ubunge kwa viti maalum. Kwa upande wa ajira tumeona mashirika mengi yakitangaza nafasi za kazi wanatoa kipaumbele kwa wanawake, kuwa iwapo mwanamke na mwanaume wote wakiwa na viwango vinavyolingana mwanamke ndiye atakaye pewa nafasi hiyo.

Kauli mbiu ya mwaka huu inatoa wito kwa watu wote kutoa ahidi kuchukua hatua mathubuti za kufikia usawa wa jinsia ifikapo mwaka 2030. Mashirika ya maendeleo kitaifa na kimataifa yanaendeleza harakati za kuhamasisha usawa wa jinsia kwa kutekeleza miradi mbali mbali. LEAT pia huwa inashiriki katika mijadala mbali mbali inayotoa elimu kwa jamii kuhusu usawa wa jinsia katika utoaji wa haki pamoja na kutekeleza miradi ya kuzuia ukatili wa jinsia.

Wewe Je?, unachukua hatua gani kuhakikisha kuwa dunia inafikai asilimia 50/50 katika elimu, uchumi, ajira, uongozi wa siasa na upatikanaji wa huduma za jamii?

Usawa wa Jinsia Unaanzia Nyumbani Kwako!

Chakua Hatua, Ahidi Usawa, Wewe ni Chanzo cha Mafanikio.

 

No comments:

Post a Comment