Wednesday, February 24, 2016

WANAKIJIJI WAKAMATA MBAO ZENYE THAMANI YA SHILINGI MILIONI 9

Bwana Chuki Mduda akiwa amesimama mbele ya mzigo wa mbao 298, zilizo vunwa bila kibali, mbao hizo zilivunwa katika msitu wa asili wa Gangalamtumba katika kijiji cha Mfyome


Wananchi wa kijiji cha Mfyome kata ya Kiwere, katika halmashauri ya Iringa Vijijini wamekamata mzigo wa mbao 298 zilizo vunwa isivyo halali katika msitu wa asili wa Gangalamtumba, hivyo kusababisha uharibifu wa mazingira.

Ukamatwaji wa mbao hizo ni matokeo ya mafunzo ya mradi wa Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili, maradi unaotekelezwa na Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).

Mwishoni mwa mwezi Januari wananchi wa kijiji hicho walikamata mbao hizo, mtuhumiwa alikimbia na kutelekeza mzigo huo. Viongozi wa kijiji waliamua kutaifisha mbao hizo na kuelekeza kuwa zitatumika kutengeneza madawati ilikukabiliana na changamoto ya upungufu wa madawati inayoikabili jamii hiyo.

Kwa upande wake Mjumbe wa Timu ya Ufuatiliaji Uwajibikaji katika Jamii kwa ngazi ya Wilaya, ambaye ni mkazi wa kijiji hicho bwana Chuki Mduda alisema kuwa mafunzo ya Ushiriki wa Wananchi katika Usimamaizi wa Maliasili yameleta hamasa na mwamko mkubwa katika jamii kwakuwa wananchi sasa wananshiriki kikamilifu na matokeo ya kukamatwa kwa mbao hizo ni kielelezo cha ari ya uwajibikaji.

Alisema mbao hizo zilivunwa kutoka katika msitu wa asili wa Gangalamtumba, alidai kuwa tayari eneo kubwa la msitu huo limeathiriwa vibaya.

“Tangu tulipohudhuria mafunzo haya kumekuwa na mabadiliko makubwa, tume hamasika kulinda maliasili zetu, na tumejipanga kupambana na wote watakao vuna rasilimali misitu bila ya kibali, tutawachukulia hatua za kisheria, ikiwa ni pamoja na kuwanyang’anya rasilimali watakazo kamatwa nazo na watalipa faini kulingana na sheria za kijiji”, alisema Mduda.


No comments:

Post a Comment