Monday, February 1, 2016

IRINGA WAPONGEZA MRADI, WAPANDA MITI 45,000 KUKABILIANA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA


Wakazi wa kijiji cha Kiwere wilaya ya Iringa vijijini wametoa shukrani zao za dhati kwa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) na kwa Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) kwa kuendesha mradi wa ‘Ushiriki wa wananchi katika Kusimamia Maliasili’.

Akiongea wakati wa tathimini ya mafunzo ya mradi, kiongozi wa kikundi cha kuhifadhi mazingira (Kiwere Hifadhi Mazingira), Hamza Chang’a alisema, kabla ya mradi alikuwa na uelewa wa kawaida kuwa ukataji miti hauruhusiwi kwa kuwa unaharibu mazingira, hakuelewa kuwa wananchi wanao wajibu wa kulinda mazingira na maliasili kwa maendeleo endelevu na kuwa jambo hilo limeelezwa katika katiba ya nchi.

“Nilipoona watu wakikata miti, niliona ni jambo la kawaida, sikufahamu athari ya muda mrefu itokanayo na vitendo hivyo, namna vianavyo athiri ubora wa maisha ya sasa na vizazi vijavyo. Nilidhani ni wajibu wa kamati ya maliasili ya kijiji na viongozi wa kijiji kulinda maliasili, aliongeza.

Alisema mafunzo yamemwongeza ufahamu, yamebadilisha mtazamo kuhusu usimamizi wa maliasili, na ameanza kutumia ujuzi wake kwa vitendo kama mwananchi muwajibikaji.

Aliendelea kusema kuwa amepata dhana kamili ya ushiriki katika michakato wa maendeleo hivyo atajitolea kushawishi, kufanya kampeni na kufuatilia utekelezaji wa huduma za jamii.

Baada ya mafunzo, Chang’a na wenzake 16 waliunda kikundi cha kuhifadhi mazingira na katika kipindi cha miezi minne wamepanda zaidi ya miti 45,000 aina ya Mijoholo na Mikaratusi. Miti hiyo itapandwa katika eneo la msitu wa Msuni lilio haribiwa kutokana na ukataji miti hovyo na uchomaji mkaa.

Kwa upande wake Devotha Mihayo alisema, amejifunza kuwa uharibifu wa mazingira una athari kubwa kwa jamii hususan kwa wanawake. Unaathiri vyanzo vya maji, unasababisha ukame na njaa katika jamii. ‘Iwapo vyanzo vya maji vita haribiwa tutalazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji, ambapo utatupotezea muda na kuweka maisha na afya zetu hatarini’ alisisitiza.

Alisema kuwa katika jamii yake hawaja wahi kushuhudia ukame kwa kuwa mvua inanyesha kwa wakati, lakini mafunzo yame watahadharisha kuhusu ukataji miti ambao unaweza kusababisha mabadiliko ya hali ya hewa hivyo kuleta mazalia ya mbu na kusababisha ugonjwa wa malaria. “Kila mmoja katika jamii yetu anahamasishwa kushiriki katika utunzaji wa mazingira wakati huo huo tukitunza afya zetu, zaidi ya hapo tuna hamasisha watoto kutoa taarifa za shughuli za uharibifu wa mazingira ilituchukue hatua za kuzuia haraka iwezekanavyo, alisema.

Naye Mashaka Kalinga Katibu Mtendaji wa asasi ya kiraia ya MJUMIKK, alithibitisha kuwa kijiji kimefanya jitihada nyingi za kuanzaisha uvunaji endelevu ili kuongeza mapato na kuhakikisha kuwa mapato yanayopatikana yananufaisha jamii. Zaidi ya hayo, serikali ya kijiji imezuia uchomaji mkaa, uvunaji miti usio endelevu, wameimarisha ulinzi na wanahamasisha wananchi kushiriki jitihada hizo.

Jumla ya wananchi 75 kutoka katika kamati za vijiji zikiwemo, kamati ya ardhi, kamati za mazingira na maliasili, baraza la ardhi, kamati ya maliasili ya wilaya na wawakilishi wa wananchi kutoka makundi mbalimbali, walihudhuria mafunzo ya Mradi wa Ushiriki wa wananchi katika Kusimamia Maliasili.

Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira kinatekeleza mradi wa miaka minne unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani, mradi wa Ushiriki wa Wananchi katika Kusimamia Maliasili, katika wilaya za Iringa na Mufindi, mkoani Iringa. Mradi ulianza mwaka 2014 na unatarajiwa kumalizika mwaka 2017.

 
Kiongozi wa ‘Kiwere Hifadhi Mazingira’, Hamza Chang’a na mwanakikundi Bruno Mpagama wakionesha sehemu ya miti 45,000, waliyo otesha katika bustani kijijini Kiwere
 
Katika picha ya pamoja ni baadhi ya washiriki wa mradi wa Ushiriki wa Wananchi katika Kusimamia Maliasili, Kijijini Kiwere

No comments:

Post a Comment