Saturday, June 4, 2016

VIKUNDI 32 VYA UFUGAJI NYUKI KATIKA WILAYA ZA IRINGA NA MUFINDI VYA PATIWA ELIMU YA UJASIRIAMALI


Vikundi 32 vya ufugaji nyuki vya wilaya za Iringa na Mufindi vyapatiwa elimu ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki ili kuwawezesha kufanya ujasiriamali bora na kuleta tija katika soko shindani la bidhaa za nyuki (asali na nta).

Vikundi hivyo vilipatiwa mafunzo ya siku tatu na Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) kwa kushirikiana na Mtaalamu wa kujitegemea wa Ujasiriamali, Rogasian Mtana. Wanavikundi hao walipatiwa mafunzo kwa nyakati tofauti ambapo walijengewa uwezo wa kutambua asali iliyoiva, urinaji bora (uvunaji wa asali) unaofuata njia za kitaalam na rafiki kwa mazingira pamoja na njia bora za uchakataji asali ilikukidhi viwango bora vya asali na nta.

Katika kuhakikisha kuwa vikundi hivyo vinapata masoko ya asali na nta, ndani na nje ya Tanzania, vikundi vilielekezwa njia sahihi za kufuata ilikupata vibali vya usindikaji ikiwa ni pamoja na kupata kibali kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Chakula na Dawa (TFDA).
Pia walifundishwa namna bora ya uhifadhi, usindikaji na ubinifu wa lebo na alama ambazo hutoa taarifa juu ya viambato, viwango vya ubora, uzito wa asali, tarehe ya uchakataji na ufungashaji na mahali ilipotoka.
Katika kuhakikisha kuwa asali na nta zinaendelea kuwa katika viwango vya juu vya ubora, vikundi vilifundisha njia sahihi za usafirishaji wa bidhaa zao. Pia walijifunza namna ya kutafuta masoko ikiwa ni pamoja na utoaji huduma bora kwa mteja, pia walipewa orodha ya makampuni yanayofanya biashara ya asali na nta.
Ilikuwasaidia wanavikundi kuwa na biashara endelevu na zenye tija, wawezeshaji wa mafunzo walitoa mafunzo ya utunzaji wa fedha na kumbukumbu. Wanavikundi pia walielekezwa namna ya kuandika katiba za vikundi vyao iliwaweze kuvisajili kisheria na kufungua akaunti za benki kwaajili ya kutunza fedha zao.
Mafunzo hayo ya ujasiriamali katika mazao ya nyuki ndio yamekamilisha programu ya mafunzo ya ufugaji nyuki. Awali vikundi hivyo vilipatiwa mafunzo ya ufugaji nyuki pamoja na kupewa mizinga ya kufugia nyuki na vifaa vya kujikinga na nyuki. Kila wilaya ina vikundi 16 ambapo kila kikundi kina watu 22.
Kukamilika kwa mafunzo ya ufugaji nyuki kutasaidia kufika malengo ya mradi ya kupunguza utegemezi wa rasilimali misitu na wanyamapori kwa jamii zinazoishi karibu na rasilimali hizo; kwa kuwapatia vyanzo mbadala vya mapato.
LEAT inatekeleza mradi wa ‘Ushiriki wa Wananchi katika Usimamizi wa Maliasili’, kwa kushirikiana na Asasi za kiraia za MUVIMA na ASH-TECH kwa wilaya ya Mufindi; na Asasi za MJUMIKK na MBOMIPA kwa wilaya ya Iringa. Mradi unatekelezwa katika vijiji 32 kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID).


Wanawake walioamua kufanya ujasiriamali wa mazao ya nyuki -wakiwa katika kazi za kikundi wakati wa mafunzo
 
 
Wanakikundi wakijadili jinsi ya kutafuta masoko na mbinu bora za utoaji huduma kwa mteja
 
Tutatoka tu: Wanakikundi wakijadili usanifu wa lebo nzuri kwaajili ya asali
 

Mwanakikundi akiangalia chujio ya asali wakati wa mafunzo
 
 
 
 
 Ubunifu: Mmoja wa wanakikundi akisaniu lebo ya asali wakati wa kazi za kikundi za majaribio
Mwanakikundi akichora lebo kwaajili ya vifungashio vya asali
 
 
Washiriki wa mafunzo ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki wilayani Mufindi
 Mshiriki wa mafunzo akiangalia chujio ya asali
Katika picha ya pamoja ni Wanavikundi vya ufugaji nyuki walio hudhuria mafunzo ya ujasiriamali wa mazao ya nyuki wilayani Iringa
 

No comments:

Post a Comment