Wednesday, December 2, 2009

MCHANGO WA SERA KATIKA KUSABABISHA MABADILIKO YA TABIA-NCHI TANZANIA

Emmanuel S. Massawe

Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira - LEAT



Utangulizi

Mabadiliko ya tabia-nchi ni maafa yaliyo dhahiri kisayansi kwa sasa. Imethibitishwa na wanasayansi mbalimbali duniani kuwa maafa haya (mabadiliko ya tabia-nchi) yanahatarisha maisha ya wanadamu na viumbe hai wengine. Jambo muhimu la kutilia maanani ni kuwa mabadiliko ya tabia-nchi yamesababishwa na mwanadamu kwa kutekeleza mipango ilokusudiwa kuchagiza maendeleo ya kiuchumi.

Nchi zote za ulimwenguni zimekuwa zikitekeleza na kuweka kipaumbele shughuli zinazoleta maendeleo bila kutilia maanani mazingira na vizazi vijavyo. Mabadiliko ya tabia-nchi yanasababishwa kwa kiasi kikubwa na vitendo vya kuchoma nishati asilia, kubadilisha eneo la misitu kuwa jangwa na kufanya shughuli zinazozalisha gesijoto kwa wingi. Nishati asilia inapochomwa huzalisha gesijoto ambayo huenda angani na kutuama/kuelea katika sehemu ya anga.

Hii husababisha kuongezeka kwa joto duniani. Uzalishaji wa gesijoto kwa wingi na kasi ya kugeuza misitu kuwa jangwa hupunguza uwezo wa misitu kunyonya hewa ukaa na gesi nyingine, hivyo kuharibu uwiano wa asili angani na kupelekea kuwepo kwa mlundikano wa gesijoto angani. Kwa sasa mlundikano wa hewa ukaa angani inaaminika umefikia kiwango cha juu kabisa. Hivyo kuna uhitaji mkubwa wa kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa na gesijoto duniani.

Nchi zenye maendeleo ya viwanda (kwa mfano, nchi za Ulaya, China, India na Marekani) zimechangia/zinachangia kwa kiasi kikubwa mabadiliko ya tabia-nchi kutokana na gesijoto zinazozalishwa kutoka viwandani na katika sekta ya usafiri. Nchi zinazoendelea zimechangia kwa kiasi kidogo sana. Ni asilimia 17 tu ndio inazalishwa na nchi zinazoendelea kutokana na kupotea kwa misitu kunakotokana na uvunaji holela.

Bara lote la Afrika linachangia asilimia 3 tu ya gesijoto inayozalishwa duniani. Ijapokuwa nchi zinazoendelea zinachangia kidogo sana mabadiliko ya tabia-nchi (hasa zile za Afrika), ndizo zinazoathrika sana kutokana na athari za mabadiliko ya tabia-nchi. Nchi tajiri duniani haziathiriki sana ukilinganisha na nchi maskini.

Mabadiliko ya tabia-nchi ni maafa yaliyo bayana kabisa na yenye kuviza maendeleo ya mwanadamu. Mathalani, maafa haya yameathiri kwa kiasi fulani jitihada za jumuiya za kimataifa kupunguza umaskini duniani na kutimiza Malengo ya Milenia. Ni dhahiri kuwa kwa sasa, mabadiliko ya tabia-nchi yanaathiri misingi ya maisha duniani. Yanaathiri rasilimali na mifumo-hai ambayo wanadamu tunategemea kwa chakula na maji, uzalishaji wa misitu yetu na maeneo ya kilimo.

Athari ziletwazo na mabadiliko ya tabia-nchi

Kutokana na Ripoti ya Nne ya Jopo la Wataalamu la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Mabadiliko ya Tabia-nchi (IPCC) iliyotolewa mwishoni mwa 2007, wastani wa joto duniani umeongezeka kwa digrii za sentigredi 0.74 toka mapinduzi ya viwanda kuanzishwa.

Ripoti hii imeonesha kuwa kati ya 1970 na 2004, mlundikano wa gesijoto angani umeongezeka kwa asilimia 70, ambapo mlundikano wa hewa ukaa umeongezeka kwa asilimia 80 kwa kipindi hicho. Ni dhahiri kuwa kadiri mlundikano wa hewa ukaa na gesijoto angani unavyoongezeka, ndivyo maafa na athari za mabadiliko ya tabia-nchi yanavyoongezeka kwa nchi maskini.

Kutokana na haya, tafiti zimethibitisha kuwa:-

· Kumetokea maafa ya ukame duniani ambayo yameathiri upatikanaji wa chakula kwa binadamu na wanyama. Pia yatapelekea kushuka kwa uzalishaji wa mazao kwa kilimo kinachotegemea mvua kwa asilimia 50. Hii itaathiri upatikanaji wa chakula na kuwepo kwa baa la njaa.

· Kuongezeka kwa matukio ya mafuriko makubwa ambayo yameathiri mifumo-hai na kusababisha vifo vya watu na wanyama na kuharibu miundo-mbinu.

· Kumetokea vipindi virefu vya joto kali na ukame vilivyopunguza upatikanaji wa maji safi kwa kunywa na kilimo.

· Kumetokea mioto hatari iliyoteketeza misitu ambayo mwanadamu anaitegemea kwa nishati kuni, hewa safi (oksijeni) na uoto wa asili.

· Kumekuwepo ongezeko la joto duniani linaliathiri maisha ya kawaida ya mwanadamu.

· Kumekuwa na ongezeko la magonjwa ya kitropiki, mathalani, malaria ambayo yamechagizwa na kuongezeka kwa mazalio ya mbu kutokana na kuongezeka kwa joto.

· Kuyeyuka kwa theluji kwenye safu za milima mirefu na maeneo yaliyo katika ncha za dunia kunakosababisha kupanda kwa kina cha bahari.

· Kina cha bahari kuongezeka kwa baadhi ya maeneo duniani na kupelekea eneo fulani la visiwa au nchi kavu kufunikwa na maji. Hii inahatarisha maisha ya watu waishio visiwani kwani kama hali ikiendelea visiwa vyote vyaweza kufunikwa na maji ya bahari. Pia kuongezeka kwa kina cha bahari kutapunguza kuwepo kwa maji baridi kwa ajili ya matumizi ya binadamu kunakotokana na kuongezeka kwa maji ya chumvi katika nchi kavu (Salt water intrusion).

Athari na maafa haya yamethibitishwa kutokea na kuhusiana na mabadiliko ya tabia-nchi. Yanaendelea kutokea na kuathiri baadhi ya maeneo ya dunia kwa sasa. Jitihada mahsusi na za haraka zinahitaji kuchukuliwa ili kuwakinga watu na athari na kupunguza visababishi vya mabadiliko ya tabia-nchi.


Sera mbali mbali na mchango wake katika kusababisha Mabadiliko ya Tabia-Nchi

Sera ni chombo cha utekelezaji wa Sheria, mipango ya maendeleo, na mikakati mbalimbali. Sera hazina nguvu ya kisheria lakini zinaweka msingi wa kutunga au kurekebisha Sheria. Sera hutoa maelekezo na hatua za kuchukua katika utekelezaji wake. Serikali hutumia Sera mbalimbali kutekeleza mipango na mikakati ya maendeleo.

Utekelezaji wa Sera kadha wa kadha unatakiwa kuleta matunda bora kwa jamii kwa kuchagiza maendeleo na kupunguza umaskini. Utekelezaji wa Sera unaweza kuwa wa manufaa kwa jamii au ukaiathiri jamii kwa namna moja au nyingine. Malengo na maudhui ya Sera mbalimbali hayatakiwi kugongana kwani zitaleta madhara kwa jamii.

Sera zinazoratibu sekta moja zinatakiwa zishirikiane kimaudhui na kiutekelezaji ili kuratibu vyema shughuli za utekelezaji wa mipango na mikakati ya maendeleo. Sera zinatakiwa zilete maendeleo endelevu bila kuathiri mahitaji na maslahi ya vizazi vijavyo. Utekelezaji wa Sera mbalimbali huchangia kwa namna moja au nyingine kuleta mabadiliko ya tabia-nchi. Sera hizi na jinsi zinavyochangia kuwepo kwa mabadiliko ya tabia-nchi zinaelezewa hapa chini kinagaubaga.

Sera ya Taifa ya Misitu, 1998

Sera ya Taifa ya Misitu nchini Tanzania ilitangazwa mwaka 1953. Sera hii imekuwa inarekebishwa mara kadhaa pale uhitaji wa kuirekebisha ulipotokea. Lengo la kuwa na Sera hii ni kuainisha na kuratibu namna ambavyo rasilimali ya misitu na miti inaweza kutumika kwa misingi endelevu ili kukidhi mahitaji na matakwa ya jamii na taifa.

Moja ya madhumuni ya sekta ya misitu ni kupanua ajira na kuongeza pato la fedha za kigeni kutokana na maendeleo endelevu katika viwanda vinavyojikita kwenye misitu na biashara. Ili kufikia dhumuni hili serikali inabudi kufungua milango na kuruhusu uwekezaji katika sekta ya misitu.

Ili uwekezaji katika sekta ya misitu ulete na kuongeza fedha za kigeni ni lazima uvunaji wa rasilimali misitu na miti ufanyike kwa kiwango kikubwa ili kuleta manufaa ya kibiashara. Uvunaji wa misitu unatakiwa kuwa endelevu kwa kutilia maanani rasilimali misitu na miti zilizoko nchini. Hili linachangia kuwepo kwa mabadiliko ya tabia-nchi kwani miti huvunwa kwa wingi sana ili kuongeza pato la fedha za kigeni.


Tutambue kuwa miti hufyonza hewa ukaa kwa ajili ya kutengenezea chakula. Lakini uvunaji wa kiwango kikubwa wa misitu na rasilimali miti huacha eneo kubwa la nchi kuwa jangwa. Hii inamaanisha kuwa hewa ukaa na gesijoto zinalundikana angani na kusababisha mabadiliko ya tabia-nchi.

Sera ya Taifa ya Mazingira, 1997

Sera hii ilipitishwa na serikali kwa madhumuni ya kutoa ufafanuzi na maelekezo ya namna ya kuratibu shughuli za kuhifadhi na kuyalinda mazingira. Baadhi ya malengo ya Sera ya Taifa ya Mazingira ni kuhakikisha upatikanaji, ulinzi na matumizi sawa ya rasilimali kwa ajili ya mahitaji muhimu ya vizazi vya sasa na vijavyo bila ya kuharibu mazingira au kuhatarisha afya au usalama wa binadamu.

Pia, kuzuia kudhibiti na uharibifu wa ardhi, maji, mimea na hewa ambavyo ndivyo vinashikilia mifumo ya maisha yetu. Malengo haya yanatakiwa yatekelezwe kikamilifu na yasimamiwe na watendaji makini. Mapungufu au uzembe katika kuratibu na kutekeleza malengo ya Sera ya Mazingira yatapelekea uharibifu wa mazingira na uzalishaji wa hewa ukaa na gesijoto kwa wingi.

Ili kuyalinda na kuyatunza mazingira, hatuna budi kukusanya na kutupa taka ngumu na taka-kimiminika tunazozalisha kila siku kwa uangalifu bila kuathiri mazingira na afya za wanadamu. Kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Mazingira, taka ngumu na taka-kimiminika hutupwa katika dampo lililofunguliwa na kusimamiwa kitaalamu.

Taka zinapotupwa katika dampo hulundikaka na kuoza. Taka hizi huzalisha gesijoto aina ya Methane ambayo husababisha mabadiliko ya tabia-nchi. Ni kwa minajili hii utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mazingira inachangia kuwepo kwa mabadiliko ya tabia-nchi.

Sera ya Wanyamapori, 2007

Sera hii iliundwa kwa lengo la kuhifadhi, kulinda na kuratibu matumizi endelevu ya wanyamapori na maeneo ya ardhi-oevu. Utekelezaji wa Sera hii hauna mchango wa moja kwa moja kwa mabadiliko ya tabia-nchi. Ila uhifadhi wa wanyamapori huchangia kwa namna moja au nyingine kuwepo kwa mabadiliko ya tabia-nchi. Vinyesi vya wanyamapori na uwindaji haramu wa kuwaua hovyo wanyamapori kwa kusaka ngozi au pembe za ndovu huzalisha hewa ukaa na gesijoto ambavyo huchangia mabadiliko ya tabia-nchi.

Sera ya Taifa ya Nishati, 2003

Sera hii inanuia kuhakikisha kuwepo na upatikanaji wa nishati ya kudumu na ya bei nafuu na kuwepo kwa matumizi endelevu ya nishati ili kuchagiza maendeleo ya kiuchumi. Upatikanaji wa nishati ya uhakika na ya kudumu unahitaji kutekelezwa kwa shughuli za ufuaji au uzalishaji wa nishati kwa njia tanzu tofauti. Nishati huzalishwa kwa kutumia maji, mionzi ya jua, upepo, petroli, nuklia na mimea (kwa mfano, bayo-dizeli). Uzalishaji nishati kwa kutumia njia hizi kunaweza kukasababisha mabadiliko ya tabia-nchi.

Mfano hai ni kuzalisha nishati ya bayo-dizeli kwa kutumia mibono. Uzalishaji wa nishati kwa njia hii hutumia maeneo makubwa ya mashamba ambayo huanzishwa kwa kukata miti ili kupata eneo la wazi la kulima mibono. Kwa kukata miti uoto wa asili unaofyonza hewa ukaa utaondolewa na kupelekea kuwepo kwa mlundikano mkubwa wa hewa ukaa na gesijoto angani.

Pia, ufuaji umeme kwa kutumia petroli kunapelekea kupata nishati bora kwa matumizi ya uzalishaji na kuleta maendeleo. Ila matumizi ya petroli kwa kuzalisha umeme kunachangia kwa kiwango kikubwa kuongezeka kwa hewa ukaa duniani. Kwa kutekeleza Sera ya Taifa ya nishati kuzalisha nishati kusipotilia maanani athari za mazingira zinazoletwa na matumizi ya njia husika ya uzalishaji umeme/nishati kunachangia mabadiliko ya tabia-nchi.

Sera ya Taifa ya Kilimo kwanza

Baadhi ya mazao ya nafaka hasa yale yalimwayo katika maji mengi yanachangia kuongezeka kwa gesi joto iitwayo methane. Hii inatokana na kupungua kwa hewa ya oksijeni kwenye udongo kadri maji yanavyokuwa mengi na kusababisha kuoza kwa masalia ya mimea na wanyama. Mimea kama ya mpunga haiwezi kushikilia kabon kwenye udongo kukiwa hakuna oksijen, na hii husababisha bakteria walioko ardhini kutengeneza methane. Hii gesi joto inayotengenezwa huachiliwa angani kwa njia ya upumuaji unaofanywa na mimea ya mpunga. Hivyo husababisha kuongezeka kwa gesi joto angani.

Hitimisho

Utekelezaji wa Sera mbalimbali za Taifa unalenga kuchagiza maendeleo ya kiuchumi na kupunguza umaskini. Ni dhahiri kuwa Sera huchangia kuwepo kwa mabadiliko ya tabia-nchi. Hivyo, utekelezaji wa Sera hizi unatakiwa ufanyike kwa umakini wa hali ya juu ukizingatia masuala ya mazingira na athari za utekelezaji wake.

No comments:

Post a Comment